Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba amesema mtu 
aliyemtishia kwa bastola aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
 Michezo, Nape Nnauye si askari wa Jeshi la Polisi, lakini 
ameshapatikana na atashughulikiwa kwa mujibu wa utaratibu wa ulinzi na 
usalama.
Mwigulu alisema hayo baada ya kufungua mkutano wa kazi wa 
mwaka wa maofisa waandamizi wa polisi, makamanda wa mikoa na wakuu wa 
vikosi wa Jeshi la Polisi ambao unafanyika mjini Dodoma. “Ameshapatikana (aliyemtishia Nape) na atashughulikiwa kwa 
mujibu wa taratibu za ulinzi na usalama ambazo zimekuwa zikifanyika 
ndani, lakini hazitangazwi,” alisema.
Hata hivyo, Mwigulu alikataa kuelezea kwa undani kuhusu mtu
 huyo kwa kubainisha anatoka taasisi gani wala jina la mtuhumiwa kwa 
madai kuwa ni kwa sababu ya usalama wake.
Mtu huyo alifanya kitendo hicho wakati Nape, ambaye alikuwa
 Waziri wa Habari, alipokuwa anaelekea Hoteli ya Protea alikopanga 
kuzungumza na waandishi wa habari baada ya mbunge huyo wa Mtama kuachwa 
katika mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri.
Mtu huyo alikuwa pamoja na wenzake wawili ambao kwa pamoja 
walikuwa wakimlazimisha arudi kwenye gari lake na kuondoka, lakini Nape 
alibisha na ndipo mtu huyo aliporudi nyuma, kuchomoa bastola kutoka 
kiunoni na kisha kumtishia kabla ya kutulizwa na mwenzake.
Watu hao walitoweka eneo hilo muda mfupi baadaye.
Siku moja baada ya tukio hilo Mwigulu alimwagiza Mkuu wa Jeshi la Polisi, Ernest Mangu kumtafuta mtu huyo.
Mwigulu aliandika katika ukurasa wake wa twitter akisema:
“Mh Nape sio jambazi, hana record za uhalifu. Kitendo cha 
kutolewa bastola si cha Kitanzania na si cha kiaskari. Nimemuagiza IGP 
achukue hatua.” Tukio hilo lilitokea siku chache baada ya RC Paul Makonda 
kuvamia kituo cha televisheni cha kampuni ya Clouds Media, akiwa na 
askari wenye silaha za moto na kulazimisha arekodiwe mahojiano baina ya 
watangazaji wa kipindi cha Shirika la Wambeya Duniani (Shilawadu) na 
mwanamke anayedai kuzaa na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat
 Gwajima, ambaye ameibukia kuwa mpinzani wa kiongozi huyo.
Hadi sasa, Jeshi la Polisi halijaeleza kuhusu askari hao waliojumuika kufanikisha uvamizi huo.
 

 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni